Wafilipi Mlango 3 Philippians

Wafilipi 3:1 Philippians 3:1

Hatimaye, ndugu zangu, furahini katika Bwana. Kuwaandikieni mambo yale yale hakuniudhi mimi, bali kutawafaa ninyi.

Wafilipi 3:2 Philippians 3:2

Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao.

Wafilipi 3:3 Philippians 3:3

Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili.

Wafilipi 3:4 Philippians 3:4

Walakini mimi ningeweza kuutumainia mwili. Mtu ye yote akijiona kuwa anayo sababu ya kuutumainia mwili, mimi zaidi.

Wafilipi 3:5 Philippians 3:5

Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo,

Wafilipi 3:6 Philippians 3:6

kwa habari ya juhudi, mwenye kuliudhi Kanisa, kwa habari ya haki ipatikanayo kwa sheria sikuwa na hatia.

Wafilipi 3:7 Philippians 3:7

Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.

Wafilipi 3:8 Philippians 3:8

Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo;

Wafilipi 3:9 Philippians 3:9

tena nionekane katika yeye, nisiwe na haki yangu mwenyewe ipatikanayo kwa sheria, bali ile ipatikanayo kwa imani iliyo katika Kristo, haki ile itokayo kwa Mungu, kwa imani;

Wafilipi 3:10 Philippians 3:10

ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake;

Wafilipi 3:11 Philippians 3:11

ili nipate kwa njia yo yote kuifikia kiyama ya wafu.

Wafilipi 3:12 Philippians 3:12

Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu.

Wafilipi 3:13 Philippians 3:13

Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele;

Wafilipi 3:14 Philippians 3:14

nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.

Wafilipi 3:15 Philippians 3:15

Basi sisi tulio wakamilifu na tuwaze hayo; na hata mkiwaza mengine katika jambo lo lote, Mungu atawafunulia hilo nalo.

Wafilipi 3:16 Philippians 3:16

Lakini, hapo tulipofika na tuenende katika lilo hilo.

Wafilipi 3:17 Philippians 3:17

Ndugu zangu, mnifuate mimi, mkawatazame wao waendao kwa kuufuata mfano tuliowapa ninyi.

Wafilipi 3:18 Philippians 3:18

Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo;

Wafilipi 3:19 Philippians 3:19

mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani.

Wafilipi 3:20 Philippians 3:20

Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo;

Wafilipi 3:21 Philippians 3:21

atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.