Filemoni Mlango 1 Philemon

Filemoni 1:1 Philemon 1:1

Paulo, mfungwa wa Kristo Yesu, na Timotheo aliye ndugu yetu, kwa Filemoni mpendwa wetu, mtenda kazi pamoja nasi,

Filemoni 1:2 Philemon 1:2

na kwa Afia, ndugu yetu, na kwa Arkipo askari mwenzetu, na kwa kanisa lililo katika nyumba yako.

Filemoni 1:3 Philemon 1:3

Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu, Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.

Filemoni 1:4 Philemon 1:4

Namshukuru Mungu wangu sikuzote, nikikukumbuka katika maombi yangu;

Filemoni 1:5 Philemon 1:5

nikisikia habari za upendo wako na imani uliyo nayo kwa Bwana Yesu na kwa watakatifu wote;

Filemoni 1:6 Philemon 1:6

ili kwamba ushirika wa imani yako ufanye kazi yake, katika ujuzi wa kila kitu chema kilicho kwetu, katika Kristo.

Filemoni 1:7 Philemon 1:7

Maana nalikuwa na furaha nyingi na faraja kwa sababu ya upendo wako, kwa kuwa mioyo ya watakatifu imeburudishwa nawe, ndugu yangu.

Filemoni 1:8 Philemon 1:8

Kwa hiyo, nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza likupasalo;

Filemoni 1:9 Philemon 1:9

lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia.

Filemoni 1:10 Philemon 1:10

Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo;

Filemoni 1:11 Philemon 1:11

ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia;

Filemoni 1:12 Philemon 1:12

niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa;

Filemoni 1:13 Philemon 1:13

ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili.

Filemoni 1:14 Philemon 1:14

Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari.

Filemoni 1:15 Philemon 1:15

Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele;

Filemoni 1:16 Philemon 1:16

tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana.

Filemoni 1:17 Philemon 1:17

Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe.

Filemoni 1:18 Philemon 1:18

Na kama amekudhulumu, au unamwia kitu, ukiandike hicho juu yangu.

Filemoni 1:19 Philemon 1:19

Mimi Paulo nimeandika kwa mkono wangu mwenyewe, mimi nitalipa. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako.

Filemoni 1:20 Philemon 1:20

Naam, ndugu yangu, nipate faida kwako katika Bwana; uniburudishe moyo wangu katika Kristo.

Filemoni 1:21 Philemon 1:21

Kwa kuwa nakuamini kutii kwako ndiyo maana nimekuandikia, nikijua ya kuwa utafanya zaidi ya hayo nisemayo.

Filemoni 1:22 Philemon 1:22

Na pamoja na hayo uniwekee tayari mahali pa kukaa; maana nataraji ya kwamba kwa maombi yenu mtajaliwa kunipata.

Filemoni 1:23 Philemon 1:23

Epafra, aliyefungwa pamoja nami katika Kristo Yesu, akusalimu;

Filemoni 1:24 Philemon 1:24

na Marko, na Aristarko, na Dema, na Luka, watendao kazi pamoja nami.

Filemoni 1:25 Philemon 1:25

Neema ya Bwana Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu.