1 Wafalme Mlango 12 1st Kings

1 Wafalme 12:1 1stKings 12:1

Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme.

1 Wafalme 12:2 1stKings 12:2

Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri,

1 Wafalme 12:3 1stKings 12:3

wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema,

1 Wafalme 12:4 1stKings 12:4

Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia.

1 Wafalme 12:5 1stKings 12:5

Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao.

1 Wafalme 12:6 1stKings 12:6

Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa?

1 Wafalme 12:7 1stKings 12:7

Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.

1 Wafalme 12:8 1stKings 12:8

Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake.

1 Wafalme 12:9 1stKings 12:9

Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako?

1 Wafalme 12:10 1stKings 12:10

Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu.

1 Wafalme 12:11 1stKings 12:11

Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.

1 Wafalme 12:12 1stKings 12:12

Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu.

1 Wafalme 12:13 1stKings 12:13

Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa;

1 Wafalme 12:14 1stKings 12:14

akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.

1 Wafalme 12:15 1stKings 12:15

Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni.

1 Wafalme 12:16 1stKings 12:16

Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hakuwasikia, hao watu walimjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese. Haya! Nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi. Hivyo Israeli wakaenda zao hemani kwao.

1 Wafalme 12:17 1stKings 12:17

Lakini kwa habari za wana wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda, Rehoboamu aliwatawala wao.

1 Wafalme 12:18 1stKings 12:18

Ndipo mfalme Rehoboamu akampeleka Adoramu, aliyekuwa juu ya shokoa, nao Israeli wote wakampiga kwa mawe hata akafa. Mfalme Rehoboamu akafanya haraka kupanda katika gari, ili akimbilie Yerusalemu.

1 Wafalme 12:19 1stKings 12:19

Hivyo Israeli wakaasi juu ya nyumba ya Daudi hata leo.

1 Wafalme 12:20 1stKings 12:20

Ikawa, Israeli wote waliposikia ya kwamba Yeroboamu amerudi, wakapeleka watu wakamwita aje mkutanoni, wakamfanya mfalme juu ya Israeli wote; wala hapakuwa na mtu aliyeshikamana na nyumba ya Daudi, ila kabila ya Yuda peke yake.

1 Wafalme 12:21 1stKings 12:21

Hata Rehoboamu alipofika Yerusalemu, akakusanya nyumba yote ya Yuda, pamoja na kabila ya Benyamini, watu wateule mia na themanini elfu, waliokuwa watu wa vita, ili wapigane na nyumba ya Israeli, waurudishe ufalme tena kwa Rehoboamu mwana wa Sulemani.

1 Wafalme 12:22 1stKings 12:22

Lakini likaja neno la Mungu kwa Shemaya mtu wa Mungu, kusema,

1 Wafalme 12:23 1stKings 12:23

Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani, mfalme wa Yuda, na jamaa yote ya Yuda na Benyamini, na watu waliosalia, ukisema,

1 Wafalme 12:24 1stKings 12:24

Bwana asema hivi, Msiende, wala msipigane na ndugu zenu wana wa Israeli; rudini kila mtu nyumbani kwake; kwa kuwa jambo hili limetoka kwangu. Basi, wakalisikiliza neno la Bwana, wakarudi, wakaenda zao, sawasawa na neno la Bwana.

1 Wafalme 12:25 1stKings 12:25

Ndipo Yeroboamu akajenga Shekemu katika milima ya Efraimu, akakaa huko. Akatoka huko akajenga Penueli.

1 Wafalme 12:26 1stKings 12:26

Yeroboamu akasema moyoni mwake, Basi ufalme utairudia nyumba ya Daudi.

1 Wafalme 12:27 1stKings 12:27

Kama watu hawa wakipanda kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Bwana huko Yerusalemu, ndipo mioyo ya watu hawa itamrudia bwana wao, yaani Rehoboamu, mfalme wa Yuda; nao wataniua mimi, na kumrudia Rehoboamu, mfalme wa Yuda.

1 Wafalme 12:28 1stKings 12:28

Kwa hiyo mfalme akafanya shauri, akafanyiza ng'ombe wawili wa dhahabu, akawaambia watu, Ni vigumu kwenu kupanda kwenda Yerusalemu; tazama, hii ndiyo miungu yenu, enyi Israeli, iliyowapandisha kutoka nchi ya Misri.

1 Wafalme 12:29 1stKings 12:29

Akamweka mmoja katika Betheli, na wa pili akamweka katika Dani.

1 Wafalme 12:30 1stKings 12:30

Jambo hili likawa dhambi, maana watu walikwenda kuabudu mbele ya kila mmoja, hata huko Dani.

1 Wafalme 12:31 1stKings 12:31

Tena akafanya nyumba za mahali pa juu, akafanya na watu wo wote, watu wasio wa wana wa Lawi, kuwa makuhani.

1 Wafalme 12:32 1stKings 12:32

Yeroboamu akaamuru kushika sikukuu katika mwezi wa nane, siku ya kumi na tano ya mwezi, mfano wa sikukuu iliyokuwa katika Yuda, akapanda juu ili kuiendea madhabahu. Akafanya vivyo katika Betheli akiwatolea dhabihu wale ng'ombe aliowafanya; akawaweka katika Betheli wale makuhani wa mahali pa juu alipokuwa amepafanya.

1 Wafalme 12:33 1stKings 12:33

Akatoa dhabihu juu ya ile madhabahu aliyoifanya katika Betheli, siku ya kumi na tano ya mwezi wa nane, mwezi aliouwaza moyoni mwake mwenyewe; akawaamuru wana wa Israeli waishike sikukuu hiyo, akapanda kuiendea madhabahu, ili kufukiza uvumba.