2 Mambo ya Nyakati Mlango 22 2nd Chronicles

2 Mambo ya Nyakati 22:1 2ndChronicles 22:1

Nao wenyeji wa Yerusalemu walimfanya Ahazia mwanawe mdogo awe mfalme mahali pake; maana wakubwa wote wamekwisha kuuawa na kikosi cha watu waliokuja matuoni pamoja na Waarabu. Hivyo akatawala Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda.

2 Mambo ya Nyakati 22:2 2ndChronicles 22:2

Ahazia alikuwa na umri wa miaka arobaini na miwili alipoanza kutawala; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri.

2 Mambo ya Nyakati 22:3 2ndChronicles 22:3

Yeye naye akaziendea njia za nyumba ya Ahabu; kwa kuwa mamaye alikuwa mshauri wake katika kufanya maovu.

2 Mambo ya Nyakati 22:4 2ndChronicles 22:4

Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana kama nyumba ya Ahabu; kwa kuwa hao walikuwa washauri wake, alipokwisha kufa babaye, hata aangamie.

2 Mambo ya Nyakati 22:5 2ndChronicles 22:5

Naye akaenda kwa mashauri yao, akafuatana na Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli ili kupigana na Hazaeli mfalme wa Shamu huko Ramoth-Gileadi;nao Washami wakamjeruhi Yoramu.

2 Mambo ya Nyakati 22:6 2ndChronicles 22:6

Akarudi Yezreeli ili aponye jeraha walizomjeruhi huko Rama, alipopigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda ,akashuka amtazame Yoramu mwana wa Ahabu,katika Yezreeli,kwa sababu alikuwa hawezi.

2 Mambo ya Nyakati 22:7 2ndChronicles 22:7

Basi kuangamia kwake Ahazia kulitokana na Mungu, kwa vile alivyomwendea Yoramu; kwa kuwa alipofika, akatoka pamoja na Yoramu juu ya Yehu mwana wa Nimshi, ambaye Bwana alimtia mafuta ili awakatilie mbali nyumba ya Ahabu.

2 Mambo ya Nyakati 22:8 2ndChronicles 22:8

Ikawa, Yehu alipokuwa akiwafanyia hukumu nyumba ya Ahabu, aliwakuta wakuu wa Yuda, na wana wa nduguze Ahazia, wakimtumikia Ahazia, akawaua.

2 Mambo ya Nyakati 22:9 2ndChronicles 22:9

Akamtafuta Ahazia, wakamkamata, (naye alikuwa amejificha Samaria,) wakamleta kwa Yehu, wakamwua; wakamzika, kwa maana wakasema, Huyu ni mwana wa Yehoshafati, huyo aliyemtafuta Bwana kwa moyo wake wote. Wala nyumba ya Ahazia hawakuwa na uwezo wa kuushika ufalme.

2 Mambo ya Nyakati 22:10 2ndChronicles 22:10

Basi Athalia, mama wa Ahazia, alipoona ya kuwa mwanawe amekufa, akainuka, akawaangamiza wazao wote wa kifalme wa nyumba ya Yuda.

2 Mambo ya Nyakati 22:11 2ndChronicles 22:11

Ila Yehosheba, binti mfalme, akamtwaa Yoashi, mwana wa Ahazia, akamwiba miongoni mwa wana wa mfalme waliouawa, akamweka yeye na yaya wake katika chumba cha kulala. Basi Yehosheba, binti mfalme Yehoramu, mkewe Yehoyada kuhani, (naye alikuwa umbu lake Ahazia,) akaficha usoni pa Athalia, asimwue.

2 Mambo ya Nyakati 22:12 2ndChronicles 22:12

Akawako pamoja nao, amefichwa nyumbani mwa Mungu, miaka sita. Na Athalia akaitawala nchi.