2 Wakorintho Mlango 12 2nd Corinthians
2 Wakorintho 12:1 2ndCorinthians 12:1
Sina budi kujisifu, ijapokuwa haipendezi; lakini nitafikilia maono na mafunuo ya Bwana.
2 Wakorintho 12:2 2ndCorinthians 12:2
Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu.
2 Wakorintho 12:3 2ndCorinthians 12:3
Nami namjua mtu huyo, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua);
2 Wakorintho 12:4 2ndCorinthians 12:4
ya kuwa alinyakuliwa mpaka Peponi, akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene.
2 Wakorintho 12:5 2ndCorinthians 12:5
Kwa habari za mtu kama huyo nitajisifu; lakini kwa ajili ya nafsi yangu sitajisifu, isipokuwa katika habari ya udhaifu wangu.
2 Wakorintho 12:6 2ndCorinthians 12:6
Maana kama ningetaka kujisifu singekuwa mpumbavu, kwa sababu nitasema kweli. Lakini najizuia, ili mtu asinihesabie zaidi ya hayo ayaonayo kwangu au kuyasikia kwangu.
2 Wakorintho 12:7 2ndCorinthians 12:7
Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi.
2 Wakorintho 12:8 2ndCorinthians 12:8
Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke.
2 Wakorintho 12:9 2ndCorinthians 12:9
Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu.
2 Wakorintho 12:10 2ndCorinthians 12:10
Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.
2 Wakorintho 12:11 2ndCorinthians 12:11
Nimekuwa mpumbavu, ninyi mmenilazimisha. Maana ilinipasa nisifiwe na ninyi; kwa sababu sikuwa duni ya mitume walio wakuu kwa lo lote, nijapokuwa si kitu.
2 Wakorintho 12:12 2ndCorinthians 12:12
Kweli ishara za mtume zilitendwa katikati yenu katika saburi yote, kwa ishara na maajabu na miujiza.
2 Wakorintho 12:13 2ndCorinthians 12:13
Maana ni kitu gani mlichopungukiwa kuliko makanisa mengine, ila kwa kuwa mimi sikuwalemea? Mnisamehe udhalimu huu.
2 Wakorintho 12:14 2ndCorinthians 12:14
Tazama, hii ni mara ya tatu ya mimi kuwa tayari kuja kwenu, wala sitawalemea. Maana sivitafuti vitu vyenu, bali nawatafuta ninyi; maana haiwapasi watoto kuweka akiba kwa wazazi, bali wazazi kwa watoto.
2 Wakorintho 12:15 2ndCorinthians 12:15
Nami kwa furaha nyingi nitatapanya, tena nitatapanywa kwa ajili ya roho zenu. Je! Kadiri nizidivyo kuwapenda sana, ninapungukiwa kupendwa?
2 Wakorintho 12:16 2ndCorinthians 12:16
Lakini na iwe hivyo, mimi sikuwalemea; bali kwa kuwa mwerevu naliwapata kwa hila.
2 Wakorintho 12:17 2ndCorinthians 12:17
Je! Mtu ye yote niliyemtuma kwenu, kwa mtu huyo naliwatoza kitu?
2 Wakorintho 12:18 2ndCorinthians 12:18
Nalimwonya Tito, nikamtuma ndugu yule pamoja naye. Je! Tito aliwatoza kitu? Je! Hatukuenenda kwa Roho yeye yule na katika nyayo zile zile?
2 Wakorintho 12:19 2ndCorinthians 12:19
Mwadhani hata sasa ya kuwa najidhuru kwenu! Mbele za Mungu twanena katika Kristo. Na hayo yote, wapenzi, ni kwa ajili ya kuwajenga ninyi.
2 Wakorintho 12:20 2ndCorinthians 12:20
Maana nachelea, nisije nikawakuta si kama vile nitakavyo kuwakuta, nikaonekana kwenu si kama vile mtakavyo; nisije nikakuta labda fitina na wivu, na ghadhabu, na ugomvi, na masingizio, na manong'onezo, na majivuno, na ghasia;
2 Wakorintho 12:21 2ndCorinthians 12:21
nami nitakapokuja tena, Mungu wangu asije akanidhili kwenu, nami nikawasikitikia wengi waliokosa tangu hapo, wasiutubie uchafu, na uasherati, na ufisadi walioufanya.