2 Wafalme Mlango 25 2nd Kings

2 Wafalme 25:1 2ndKings 25:1

Ikawa katika mwaka wa kenda wa kutawala kwake, katika mwezi wa kumi, na siku ya kumi ya mwezi huo, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akaja, yeye na jeshi lake lote, kupigana na Yerusalemu, akapanga hema zake kuukabili; nao wakajenga ngome juu yake pande zote.

2 Wafalme 25:2 2ndKings 25:2

Basi mji huo ulihusuriwa hata mwaka wa kumi na moja wa mfalme Sedekia.

2 Wafalme 25:3 2ndKings 25:3

Siku ya kenda ya mwezi wa nne njaa ilikuwa nzito ndani ya mji, hata hapakuwa na chakula kwa watu wa nchi.

2 Wafalme 25:4 2ndKings 25:4

Ndipo mahali pakabomolewa katika ukuta wa mji, watu wote wa vita wakakimbia usiku kwa njia ya lango lililokuwa kati ya zile kuta mbili, karibu na bustani ya mfalme; (basi wale Wakaldayo walikuwa wakiuzuia mji pande zote;) mfalme akaenda kwa njia ya Araba.

2 Wafalme 25:5 2ndKings 25:5

Lakini jeshi la Wakaldayo wakamfuatia mfalme, wakampata katika nchi tambarare ya Yeriko; na jeshi lake lote walikuwa wametawanyika na kumwacha.

2 Wafalme 25:6 2ndKings 25:6

Ndipo wakamkamata mfalme, wakamchukua kwa mfalme wa Babeli huko Ribla; wakatoa hukumu juu yake.

2 Wafalme 25:7 2ndKings 25:7

Wakawaua wana wa Sedekia mbele ya macho yake, wakampofusha macho Sedekia, wakamfunga kwa pingu, wakamchukua mpaka Babeli.

2 Wafalme 25:8 2ndKings 25:8

Hata mwezi wa tano, siku ya saba ya mwezi, ndio mwaka wa kumi na kenda wa mfalme Nebukadreza, mfalme wa Babeli, Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, mtumishi wa mfalme wa Babeli, akaingia Yerusalemu.

2 Wafalme 25:9 2ndKings 25:9

Akaiteketeza nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme; na nyumba zote za Yerusalemu, naam, kila nyumba kubwa aliiteketeza kwa moto.

2 Wafalme 25:10 2ndKings 25:10

Na jeshi lote la Wakaldayo, waliokuwa pamoja na huyo amiri wa askari walinzi, wakazibomoa kuta za Yerusalemu pande zote.

2 Wafalme 25:11 2ndKings 25:11

Na mabaki ya watu waliosalia katika mji, nao wale walioasi, na kumkimbilia mfalme wa Babeli, na mabaki ya watu wote wengine, watu hao Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua mateka.

2 Wafalme 25:12 2ndKings 25:12

Lakini huyo amiri wa askari walinzi akawaacha watu walio maskini ili wawe watunza mizabibu na wakulima.

2 Wafalme 25:13 2ndKings 25:13

Na zile nguzo za shaba zilizokuwako nyumbani mwa Bwana, na matako, na ile bahari ya shaba, iliyokuwamo nyumbani mwa Bwana, Wakaldayo wakavivunja vipande vipande, wakaichukua shaba yake yote mpaka Babeli.

2 Wafalme 25:14 2ndKings 25:14

Nayo masufuria, na majembe, na makasi, na miiko, na vyombo vyote vya shaba walivyokuwa wakivitumia, wakavichukua vyote.

2 Wafalme 25:15 2ndKings 25:15

Na vyetezo, na mabakuli; vilivyokuwa vya dhahabu katika dhahabu, na vilivyokuwa vya fedha katika fedha, amiri wa askari walinzi akavichukua.

2 Wafalme 25:16 2ndKings 25:16

Zile nguzo mbili, na ile bahari moja, na yale matako, Sulemani alivyoifanyia nyumba ya Bwana; shaba ya vyombo hivyo vyote haikuwa na uzani.

2 Wafalme 25:17 2ndKings 25:17

Urefu wa nguzo moja ulikuwa dhiraa kumi na nane, na kichwa cha shaba kilikuwa juu yake; na urefu wa kichwa ulikuwa dhiraa tatu; na mapambo ya wavu na makomamanga juu ya kichwa hicho kote kote, yote yalikuwa ya shaba. Nayo nguzo ya pili ilikuwa vivyo hivyo, pamoja na ule wavu.

2 Wafalme 25:18 2ndKings 25:18

Na amiri wa askari walinzi akamtwaa Seraya, kuhani mkuu, na Sefania, kuhani wa pili, na wale walinzi watu wa mlango;

2 Wafalme 25:19 2ndKings 25:19

na katika mji akamtwaa towashi mmoja, aliyewasimamia watu wa vita; na watu watano katika wale waliosimama mbele ya mfalme, walioonekana mjini; na katibu wa jemadari wa jeshi, aliyewaandika watu wa nchi; na watu sitini katika watu wa nchi, walioonekana mjini.

2 Wafalme 25:20 2ndKings 25:20

Kisha Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawatwaa hao, akawaleta kwa mfalme wa Babeli huko Ribla.

2 Wafalme 25:21 2ndKings 25:21

Naye mfalme wa Babeli akawapiga, na kuwaua huko Ribla katika nchi ya Hamathi. Hivyo Yuda wakachukuliwa utumwani kutoka nchi yao.

2 Wafalme 25:22 2ndKings 25:22

Na kwa habari ya watu waliosalia katika nchi ya Yuda, aliowasaza Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akamweka Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani awe liwali juu yao.

2 Wafalme 25:23 2ndKings 25:23

Kisha, wakuu wote wa majeshi, wao na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babeli amemweka Gedalia kuwa liwali, wakamwendea Gedalia huko Mispa; nao ni hawa, Ishmaeli mwana wa Nethania, na Yohana mwana wa Karea, na Seraya mwana wa Tanhumethi Mnetofa, na Yezania mwana wa Mmaaka, wao na watu wao.

2 Wafalme 25:24 2ndKings 25:24

Na Gedalia akawaapia wao na watu wao, akawaambia, Msiogope kwa ajili ya watumishi wa Wakaldayo; kaeni katika nchi; mkamtumikie mfalme wa Babeli; itakuwa vyema kwenu.

2 Wafalme 25:25 2ndKings 25:25

Lakini ikawa katika mwezi wa saba Ishmaeli mwana wa Nethania, mwana wa Elishama, mmoja wa wazao wa kifalme, na watu kumi pamoja naye, wakamwendea Gedalia, wakampiga hata akafa, na hao Wayahudi na Wakaldayo waliokuwa pamoja naye huko Mispa.

2 Wafalme 25:26 2ndKings 25:26

Wakaondoka watu wote, wadogo kwa wakubwa, pamoja na wakuu wa majeshi, wakainuka kwenda Misri; kwa kuwa waliwaogopa Wakaldayo.

2 Wafalme 25:27 2ndKings 25:27

Ikawa katika mwaka wa thelathini na saba wa kuhamishwa kwake Yekonia mfalme wa Yuda ,katika mwezi wa kumi na mbili ,siku ya ishirini na saba ya mwezi ,Evil-merodaki,mfalme wa Babeli ,katika mwaka wa kwanza wa kutawala kwake,akamwinua kichwa Yekonia,mfalme wa Yuda,akamtoa gerezani.

2 Wafalme 25:28 2ndKings 25:28

Akasema naye maneno mazuri, akaweka kiti chake cha enzi juu ya viti vya enzi vya wafalme waliokuwa pamoja naye huko Babeli;

2 Wafalme 25:29 2ndKings 25:29

naye akambadilishia mavazi yake ya gerezani, akala chakula mbele yake daima, siku zote za maisha yake.

2 Wafalme 25:30 2ndKings 25:30

Na kwa posho yake, alipewa posho ya daima na mfalme, siku kwa siku sehemu, siku zote za maisha yake.