Mambo ya Walawi Mlango 19 Leviticus
Mambo ya Walawi 19:1 Leviticus 19:1
Bwana akanena na Musa, akamwambia,
Mambo ya Walawi 19:2 Leviticus 19:2
Nena na mkutano wote wa wana wa Israeli, uwaambie, Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wenu, ni mtakatifu.
Mambo ya Walawi 19:3 Leviticus 19:3
Kila mtu na amche mama yake, na baba yake, nanyi mtazitunza Sabato zangu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:4 Leviticus 19:4
Msigeuke kuandama sanamu, wala msijifanyizie miungu ya kusubu mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:5 Leviticus 19:5
Nanyi hapo mtakapomchinjia Bwana sadaka ya amani mtaisongeza ili kwamba mpate kukubaliwa.
Mambo ya Walawi 19:6 Leviticus 19:6
Italiwa siku iyo hiyo mliyoichinja, na siku ya pili yake; na kama kitu cho chote katika sadaka hiyo kilisalia hata siku ya tatu kitachomwa moto.
Mambo ya Walawi 19:7 Leviticus 19:7
Kwamba sadaka hiyo yaliwa hata kidogo siku ya tatu ni machukizo; haitakubaliwa;
Mambo ya Walawi 19:8 Leviticus 19:8
lakini kila mtu atakayekula atauchukua uovu wake mwenyewe, kwa sababu amekinajisi kitu hicho kitakatifu cha Bwana; na nafsi hiyo itakatiliwa mbali na watu wake.
Mambo ya Walawi 19:9 Leviticus 19:9
Na mtakapovuna mavuno ya nchi yenu, usivune kabisa kabisa pembe za shamba lako, wala usiyakusanye masazo ya mavuno yako;
Mambo ya Walawi 19:10 Leviticus 19:10
wala usiyakusanye masazo ya mizabibu yako, wala usiyaokote matunda ya mizabibu yako yaliyopukutika; uyaache kwa ajili ya maskini na mgeni; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:11 Leviticus 19:11
Msiibe, wala msidanganye, wala msiambiane uongo.
Mambo ya Walawi 19:12 Leviticus 19:12
Msiape uongo kwa jina langu, hata ukalinajisi jina la Mungu wako; Mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:13 Leviticus 19:13
Usimdhulumu jirani yako, wala kumnyang'anya mali yake; ijara yake aliyeajiriwa isikae kwako usiku kucha hata asubuhi.
Mambo ya Walawi 19:14 Leviticus 19:14
Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:15 Leviticus 19:15
Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki.
Mambo ya Walawi 19:16 Leviticus 19:16
Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:17 Leviticus 19:17
Usimchukie ndugu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake.
Mambo ya Walawi 19:18 Leviticus 19:18
Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako; Mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:19 Leviticus 19:19
Mtazishika amri zangu. Usiwaache wanyama wako wa mfugo wakazaana kwa namna mbalimbali; usipande shamba lako mbegu za namna mbili pamoja; wala usivae mwilini mwako nguo ya namna mbili zilizochanganywa pamoja.
Mambo ya Walawi 19:20 Leviticus 19:20
Tena mtu ye yote alalaye na mwanamke aliye mjakazi, naye ameposwa na mume, wala hakukombolewa kwa lo lote, wala hakupewa uhuru; wataadhibiwa; hawatauawa, kwa sababu huyo mwanamke hakuwa huru.
Mambo ya Walawi 19:21 Leviticus 19:21
Na huyo mume ataleta sadaka yake ya hatia aitoe kwa Bwana, hata mlangoni pa hema ya kukutania; kondoo mume kwa hiyo sadaka ya hatia.
Mambo ya Walawi 19:22 Leviticus 19:22
Kisha huyo kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, kwa huyo kondoo mume wa sadaka ya hatia mbele za Bwana, kwa ajili ya dhambi yake aliyoifanya; naye atasamehewa hiyo dhambi yake aliyoifanya.
Mambo ya Walawi 19:23 Leviticus 19:23
Nanyi hapo mtakapoingia nchi ile, mkiwa mmepanda miti ya namna zote kwa ajili ya chakula, ndipo mtayahesabu matunda yake kama ni kutotahiriwa; muda wa miaka mitatu miti hiyo itakuwa kwenu kama kutotahiriwa; matunda yake hayataliwa.
Mambo ya Walawi 19:24 Leviticus 19:24
Lakini mwaka wa nne matunda yake yote yatakuwa ni matakatifu, kwa ajili ya kumpa Bwana shukrani.
Mambo ya Walawi 19:25 Leviticus 19:25
Na katika mwaka wa tano mtakula katika matunda yake, ili ipate kuwapa maongeo yake; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:26 Leviticus 19:26
Msile kitu cho chote pamoja na damu yake; wala msifanye kuloga, wala kutumia utambuzi.
Mambo ya Walawi 19:27 Leviticus 19:27
Msinyoe denge pembe za vichwani, wala msiharibu pembe za ndevu zenu.
Mambo ya Walawi 19:28 Leviticus 19:28
Msichanje chale yo yote katika nyama ya miili yenu kwa ajili ya wafu, wala msiandike alama miilini mwenu; mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:29 Leviticus 19:29
Usimnajisi binti yako, ili kumfanya awe kahaba; isiwe hiyo nchi kuuandama ukahaba, na nchi kujawa na uovu mkuu.
Mambo ya Walawi 19:30 Leviticus 19:30
Zishikeni Sabato zangu, mpaheshimu patakatifu pangu; mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:31 Leviticus 19:31
Msiwaendee wenye pepo, wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao; Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:32 Leviticus 19:32
Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako, Mimi ndimi Bwana.
Mambo ya Walawi 19:33 Leviticus 19:33
Na mgeni akikaa pamoja nawe katika nchi yako, usimdhulumu.
Mambo ya Walawi 19:34 Leviticus 19:34
Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri; Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.
Mambo ya Walawi 19:35 Leviticus 19:35
Msifanye yasiyo haki katika hukumu, wala katika kupima, wala katika mizani, wala katika cheo.
Mambo ya Walawi 19:36 Leviticus 19:36
Mizani ya haki, vipimo vya haki, efa ya haki, hini ya haki, ndivyo mtakavyokuwa navyo. Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri.
Mambo ya Walawi 19:37 Leviticus 19:37
Zishikeni sheria zangu, na hukumu zangu, na kuzitenda. Mimi ndimi Bwana.