Kumbukumbu la Torati Mlango 17 Deuteronomy

Kumbukumbu la Torati 17:1 Deuteronomy 17:1

Usimchinjie Bwana, Mungu wako, ng'ombe wala kondoo aliye na kilema, wala neno ovu lo lote; kwa kuwa hayo ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako.

Kumbukumbu la Torati 17:2 Deuteronomy 17:2

Ikiwa ameonekana katikati yako, ndani ya malango yako mojawapo, upewayo na Bwana, Mungu wako, mtu mume au mke afanyaye yaliyo maovu machoni pa Bwana, Mungu wako, kwa kuvunja maagano yake,

Kumbukumbu la Torati 17:3 Deuteronomy 17:3

naye amekwenda kutumikia miungu mingine na kuiabudu, au jua, au mwezi, au vilivyo katika jeshi la mbinguni vyo vyote, nisivyoagiza mimi;

Kumbukumbu la Torati 17:4 Deuteronomy 17:4

ukiambiwa hayo nawe umeyasikia, ndipo utafute kwa bidii, na tazama, ikiwa ni kweli lina hakika jambo lile, kuwa yafanywa machukizo kama hayo katika Israeli;

Kumbukumbu la Torati 17:5 Deuteronomy 17:5

ndipo umchukue nje malangoni kwako, yule mtu mume, au yule mwanamke, aliyefanya jambo lile ovu; ukawapige kwa mawe, wafe.

Kumbukumbu la Torati 17:6 Deuteronomy 17:6

Huyo atakayeuawa na auawe kwa midomo ya mashahidi wawili, au mashahidi watatu; asiuawe kwa mdomo wa shahidi mmoja.

Kumbukumbu la Torati 17:7 Deuteronomy 17:7

Mikono ya wale mashahidi na iwe juu yake kwanza kwa kumwua, kisha mikono ya watu wote. Uondoe vivyo uovu katikati yako.

Kumbukumbu la Torati 17:8 Deuteronomy 17:8

Ikiwa limezuka neno lililo zito kukupita wewe, katika maamuzi kati ya damu na damu, na kati ya daawa na daawa, na kati ya pigo na pigo, nayo yashindaniwa katika malango yako; ndipo nawe uondoke, ukwee uende mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako;

Kumbukumbu la Torati 17:9 Deuteronomy 17:9

uwaendee makuhani Walawi, na mwamuzi atakayekuwako siku hizo; uwaulize; nao watakuonyesha hukumu ya maamuzi;

Kumbukumbu la Torati 17:10 Deuteronomy 17:10

nawe fanya sawasawa na hukumu watakayokuonyesha mahali hapo atakapochagua Bwana; nawe tunza kufanya kwa mfano wa yote watakayokufunza;

Kumbukumbu la Torati 17:11 Deuteronomy 17:11

kwa mfano wa sheria watakayokufunza, na kwa mfano wa hukumu watakayokuambia, fanya vivyo; usigeuke katika hukumu watakayokuonyesha, kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto.

Kumbukumbu la Torati 17:12 Deuteronomy 17:12

Na mtu afanyaye kwa kujikinai, kwa kutomsikiza kuhani asimamaye hapo kwa kumtumikia Bwana, Mungu wako, au mwamuzi, na afe mtu huyo; nawe utauondoa uovu katika Israeli.

Kumbukumbu la Torati 17:13 Deuteronomy 17:13

Na hao watu wote watasikia na kuogopa, wasifanye tena kwa kujikinai.

Kumbukumbu la Torati 17:14 Deuteronomy 17:14

Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako ukaimiliki, na kukaa humo; nawe utakaposema, Nitaweka mfalme juu yangu mfano wa mataifa yote yaliyo kando-kando yangu;

Kumbukumbu la Torati 17:15 Deuteronomy 17:15

usiache kumweka yule atakayechaguliwa na Bwana, Mungu wako, awe mfalme juu yako; umweke mmoja katika ndugu zako awe mfalme juu yako; usimtawaze mgeni juu yako, ambaye si ndugu yako.

Kumbukumbu la Torati 17:16 Deuteronomy 17:16

Ila asifanye farasi wake kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi; kwa kuwa Bwana amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile.

Kumbukumbu la Torati 17:17 Deuteronomy 17:17

Wala asijizidishie wake, ili moyo wake usikengeuke; wala asifanye fedha zake na dhahabu kuwa nyingi mno.

Kumbukumbu la Torati 17:18 Deuteronomy 17:18

Tena na iwe, zamani aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi;

Kumbukumbu la Torati 17:19 Deuteronomy 17:19

na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha Bwana, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya;

Kumbukumbu la Torati 17:20 Deuteronomy 17:20

moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake, wala asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto; ili apate kuzifanya siku zake kuwa nyingi katika ufalme wake, yeye na wanawe, katikati ya Israeli.