Kutoka Mlango 10 Exodus

Kutoka 10:1 Exodus 10:1

Bwana akamwambia Musa, Ingia wewe kwa Farao; kwa kuwa mimi nimeufanya moyo wake mzito, nipate kuzionyesha ishara zangu hizi kati yao;

Kutoka 10:2 Exodus 10:2

nawe upate kusema masikioni mwa mwanao, na masikioni mwa mjukuu wako, ni mambo gani niliyotenda juu ya Misri, na ishara zangu nilizozifanya kati yao; ili mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Kutoka 10:3 Exodus 10:3

Basi Musa na Haruni wakaingia kwa Farao, na kumwambia, Bwana, Mungu wa Waebrania, asema hivi, Je! Utakataa hata lini kujinyenyekeza mbele zangu? Wape watu wangu ruhusa waende zao, ili wanitumikie.

Kutoka 10:4 Exodus 10:4

Au, kwamba wakataa kuwapa hao watu wangu ruhusa waende zao, tazama, kesho nitaleta nzige waingie ndani ya mipaka yako;

Kutoka 10:5 Exodus 10:5

nao wataufunika uso wa nchi, mtu asipate kuona hiyo nchi; nao watakula mabaki ya hayo yaliyopona yaliyowasalia baada ya ile mvua ya mawe, watakula kila mti umeao kwa ajili yenu mashambani;

Kutoka 10:6 Exodus 10:6

na nyumba zako, na nyumba za watumishi wako, na nyumba za Wamisri wote zitajawa na nzige; mfano wake baba zako wala baba za baba zako hawakuona, tangu siku walipoanza kuwapo juu ya nchi hata hivi leo. Basi akageuka na kutoka kwa Farao.

Kutoka 10:7 Exodus 10:7

Ndipo watumishi wa Farao wakamwambia, Mtu huyu atakuwa tanzi kwetu sisi hata lini? Wape hawa watu ruhusa waende zao, wamtumikie Bwana, Mungu wao; hujatambua bado ya kuwa Misri imekwisha haribika?

Kutoka 10:8 Exodus 10:8

Musa na Haruni wakaletwa tena kwa Farao; naye akawaambia, Nendeni, mkamtumikie Bwana, Mungu wenu; lakini ni kina nani watakaokwenda?

Kutoka 10:9 Exodus 10:9

Musa akamjibu, Tutakwenda na vijana wetu na wazee wetu, na wana wetu, na binti zetu, tutakwenda na kondoo zetu na ng'ombe zetu; kwa kuwa inatupasa kumfanyia Bwana sikukuu.

Kutoka 10:10 Exodus 10:10

Lakini akawaambia, Ehe, Bwana na awe pamoja nanyi, kama nitakavyowapa ruhusa kwenda zenu pamoja na watoto wenu; angalieni, kwa kuwa pana uovu huko mbele yenu.

Kutoka 10:11 Exodus 10:11

Sivyo; endeni ninyi mlio watu wazima, mkamtumikie Bwana; kwa kuwa ndilo jambo mtakalo. Nao walifukuzwa usoni pa Farao.

Kutoka 10:12 Exodus 10:12

Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako juu ya nchi ya Misri kwa hao nzige, ili wakwee juu ya nchi ya Misri, waile mimea yote ya nchi, yaani, vyote vilivyosazwa na ile mvua ya mawe.

Kutoka 10:13 Exodus 10:13

Basi Musa akainyosha fimbo yake juu ya nchi ya Misri, na Bwana akaleta upepo kutoka mashariki juu ya nchi, mchana kutwa, na usiku kucha; kulipopambazuka ule upepo wa mashariki ukawaleta nzige.

Kutoka 10:14 Exodus 10:14

Na hao nzige wakakwea juu ya nchi yote ya Misri, wakatua ndani ya mipaka yote ya Misri, walikuwa wabaya mno; hawajakuwapo nzige kama hao majira yo yote, wala baada yao hawatakuwa wengine jinsi hiyo.

Kutoka 10:15 Exodus 10:15

Kwa kuwa waliufunika uso wote wa nchi, hata nchi iliingia giza; wakala mimea yote ya nchi, na matunda yote ya miti yaliyosazwa na ile mvua ya mawe; hapakusalia hata jani moja, mti wala mmea wa mashamba, katika nchi yote ya Misri.

Kutoka 10:16 Exodus 10:16

Ndipo Farao akawaita Musa na Haruni haraka; akasema, Nimemfanyia dhambi Bwana, Mungu wenu na ninyi pia.

Kutoka 10:17 Exodus 10:17

Basi sasa, nawasihi, nisameheni dhambi yangu mara hii moja tu, mkamwombe Bwana, Mungu wenu, aniondolee kifo hiki tu.

Kutoka 10:18 Exodus 10:18

Akatoka kwa Farao, na kumwomba Bwana.

Kutoka 10:19 Exodus 10:19

Bwana akaugeuza upepo wa magharibi wenye nguvu nyingi, ambao uliwaondoa wale nzige na kuwapeleka katika Bahari ya Shamu; hakusalia hata nzige mmoja ndani ya mipaka yote ya Misri.

Kutoka 10:20 Exodus 10:20

Lakini Bwana akaufanya ule moyo wa Farao uwe mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa waende zao.

Kutoka 10:21 Exodus 10:21

Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako kuelekea mbinguni, kuwe giza juu ya nchi ya Misri, watu wapapase-papase gizani.

Kutoka 10:22 Exodus 10:22

Basi Musa akaunyosha mkono wake kuelekea mbinguni; kukawa na giza nene katika nchi yote ya Misri muda wa siku tatu;

Kutoka 10:23 Exodus 10:23

hawakupata kuonana mtu na mwenziwe, wala hakuondoka mtu mahali alipokuwa muda wa siku tatu; lakini wana wa Israeli wote walikuwa na mwanga makaoni mwao.

Kutoka 10:24 Exodus 10:24

Farao akamwita Musa, na kumwambia, Haya, nendeni, mkamtumikie Bwana; kondoo zenu na ng'ombe zenu tu na waachwe; watoto wenu nao na waende pamoja nanyi.

Kutoka 10:25 Exodus 10:25

Musa akasema, Ni lazima utupe mikononi mwetu na wanyama wa dhabihu na wa sadaka za kuteketezwa, ili tupate kumchinjia Bwana Mungu wetu dhabihu.

Kutoka 10:26 Exodus 10:26

Makundi yetu pia watakwenda pamoja nasi; hautasalia nyuma hata ukwato mmoja; kwa maana inampasa kutwaa katika hao tupate kumtumikia Bwana, Mungu wetu; nasi hatujui, hata tutakapofika huko, ni kitu gani ambacho kwa hicho inatupasa kumtumikia Bwana.

Kutoka 10:27 Exodus 10:27

Lakini Bwana akaufanya kuwa mgumu moyo wa Farao, asikubali kuwapa ruhusa waende zao.

Kutoka 10:28 Exodus 10:28

Farao akamwambia Musa, Nenda zako, ujiangalie, usinione uso tena; kwani siku hiyo utakayoniangalia uso wangu utakufa.

Kutoka 10:29 Exodus 10:29

Musa akasema, Umenena vema; mimi sitakuangalia uso wako tena.