Mithali Mlango 13 Proverbs
Mwana mwenye hekima husikiliza mausia ya babaye; Bali mwenye dharau hasikilizi maonyo.
Mtu atakula mema kwa matunda ya kinywa chake; Bali nafsi ya mtu haini itakula jeuri.
Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; Bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu.
Nafsi ya mtu mvivu hutamani asipate kitu; Bali nafsi ya mwenye bidii itanenepeshwa.
Mwenye haki huchukia kusema uongo; Bali mtu mbaya huwa karaha, hupatwa na aibu.
Haki humlinda yeye aliye mnyofu katika njia yake; Bali ubaya humwangusha mwenye dhambi.
Kuna mtu mwenye kujitajirisha, lakini hana kitu; Kuna ajifanyaye kuwa maskini, lakini ana mali nyingi.
Dia ya nafsi ya mtu ni utajiri wake; Bali mtu maskini hasikii ogofyo lo lote.
Nuru ya mwenye haki yang'aa sana; Bali taa ya mtu mbaya itazimika.
Kiburi huleta mashindano tu; Bali hekima hukaa nao wanaoshauriana.
Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa.
Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.
Kila alidharauye neno hujiletea uharibifu; Bali yeye aiogopaye amri atapewa thawabu.
Sheria ya mwenye akili ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti.
Ufahamu mwema huleta upendeleo; Bali njia ya haini huparuza.
Kila aliye na busara hutenda kazi kwa maarifa; Bali mpumbavu hueneza upumbavu.
Mjumbe mbaya huanguka maovuni; Bali mjumbe mwaminifu ni afya.
Umaskini na fedheha zitampata yeye akataaye kurudiwa; Bali yeye aangaliaye maonyo ataheshimiwa.
Haja iliyopatikana ni tamu nafsini mwa mtu; Bali kujitenga na maovu ni chukizo kwa wapumbavu.
Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.
Uovu huwaandamia wenye dhambi; Bali mwenye haki atalipwa mema.
Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi; Na mali ya mkosaji huwa akiba kwa mwenye haki.
Chakula kingi chapatikana kwa ukulima wa maskini; Bali viko viharibiwavyo kwa sababu ya dhuluma.
Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; Bali yeye ampendaye humrudi mapema.
Mwenye haki hula akaishibisha nafsi yake; Bali tumbo la mtu mbaya litaona njaa.