Mithali Mlango 15 Proverbs
Jawabu la upole hugeuza hasira; Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.
Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri; Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.
Macho ya Bwana yako kila mahali; Yakimchunguza mbaya na mwema.
Ulimi safi ni mti wa uzima; Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo.
Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye; Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara.
Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi; Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu.
Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa; Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo.
Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.
Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali humpenda mtu afuatiaye wema.
Adhabu kali ina yeye aiachaye njia; Naye achukiaye kukemewa atakufa.
Kuzimu na Uharibifu vi wazi mbele za Bwana; Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu?
Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa; Wala yeye hawaendei wenye hekima.
Moyo wa furaha huchangamsha uso; Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.
Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa; Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu.
Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.
Kuwa na mali chache pamoja na kumcha Bwana; Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu.
Chakula cha mboga penye mapendano; Ni bora kuliko ng'ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.
Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.
Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba; Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu.
Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mpumbavu humdharau mamaye.
Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili; Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake.
Pasipo mashauri makusudi hubatilika; Bali kwa wingi wa washauri huthibithika.
Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake; Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!
Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu; Ili atoke katika kuzimu chini.
Bwana ataing'oa nyumba ya mwenye kiburi; Bali atauthibitisha mpaka wa mjane.
Mashauri mabaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maneno yapendezayo ni safi.
Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe; Bali achukiaye zawadi ataishi.
Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu; Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.
Bwana yu mbali na wasio haki; Bali huisikia sala ya mwenye haki.
Mng'ao wa macho huufurahisha moyo; Habari njema huinenepesha mifupa.
Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai Litakaa kati yao wenye hekima.
Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe; Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu.
Kumcha Bwana ni maonyo ya hekima; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.