Mithali Mlango 14 Proverbs
Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.
Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha Bwana; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau.
Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi.
Zizi ni safi ambapo hapana ng'ombe; Bali nguvu za ng'ombe zaleta faida nyingi.
Shahidi mwaminifu hatasema uongo; Bali shahidi wa uongo, pumzi zake ni uongo.
Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate; Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu.
Toka mbele ya uso wa mpumbavu, Maana hutaona kwake midomo ya maarifa.
Akili za mwenye busara ni kujua njia yake; Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu.
Wapumbavu huidharau hatia; Bali upo upendeleo kwa wenye haki.
Moyo huujua uchungu wa nafsi yake, Wala mgeni haishiriki furaha yake.
Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa; Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa.
Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.
Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo.
Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake.
Mjinga huamini kila neno; Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.
Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; Bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai.
Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa.
Wajinga hurithi upumbavu; Bali wenye busara huvikwa taji ya maarifa.
Wabaya huinama mbele ya wema, Na wasio haki malangoni mwao wenye haki.
Maskini huchukiwa hata na jirani yake; Bali tajiri ana rafiki wengi.
Amdharauye mwenzake afanya dhambi; Bali amhurumiaye maskini ana heri.
Je! Hawakosi wawazao mabaya? Bali fadhili na kweli zina wao wawazao mema.
Katika kila kazi mna faida; Bali maneno ya midomo huleta hasara tu.
Taji ya wenye hekima ni mali zao; Bali upumbavu wa wajinga ni upumbavu tu.
Shahidi wa kweli huponya nafsi za watu; Bali atoaye uongo hudanganya.
Kumcha Bwana ni tumaini imara; Watoto wake watakuwa na kimbilio.
Kumcha Bwana ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti.
Utukufu wa mfalme ni wingi wa watu wake; Bali uchache wa watu ni uharibifu wa mkuu wao.
Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; Bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu.
Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; Bali husuda ni ubovu wa mifupa.
Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; Bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu.
Mtu mbaya husukumwa chini katika kutenda mabaya kwake; Bali mwenye haki ana matumaini katika kufa kwake.
Hekima hukaa katika moyo wake mwenye ufahamu; Bali yaliyo ndani ya wapumbavu hudhihirika.
Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote.
Upendeleo wa mfalme humwelekea mtumwa atendaye kwa busara; Bali ghadhabu yake itakuwa juu yake aletaye aibu.