Mithali Mlango 12 Proverbs
Kila apendaye mafundisho hupenda maarifa; Bali yeye achukiaye kulaumiwa ni kama mnyama.
Mtu mwema atapata upendeleo kwa Bwana; Bali mtu wa hila atahukumiwa naye.
Mtu hatathibitika kwa njia ya uovu; Shina la mwenye haki halitaondolewa kamwe.
Mwanamke mwema ni taji ya mumewe; Bali aaibishaye ni kama kuoza mifupani mwake.
Mawazo ya mwenye haki ni adili; Bali mashauri ya mtu mwovu ni hadaa.
Maneno ya waovu huotea damu; Bali kinywa cha wanyofu kitawaokoa.
Waovu huangamia, hata hawako tena; Bali nyumba ya mwenye haki itasimama.
Mtu atasifiwa kwa kadiri ya akili zake; Bali mwenye moyo wa ukaidi atadharauliwa.
Afadhali mtu anayedharauliwa, ikiwa ana mtumwa, Kuliko ajisifuye, ikiwa anahitaji chakula.
Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake; Bali huruma za mtu mwovu ni ukatili.
Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele; Bali afuataye mambo ya upuzi hana ufahamu.
Asiye haki hutamani nyavu za wabaya; Bali shina lao wenye haki huleta matunda.
Katika kosa la midomo kuna mtego kwa mbaya; Bali mwenye haki atatoka katika taabu.
Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake; Na atarudishiwa matendo ya mikono yake.
Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.
Ghadhabu ya mpumbavu hujulika mara; Bali mtu mwerevu husitiri aibu.
Atamkaye maneno ya kweli hufunua haki; Bali shahidi wa uongo hutamka hila.
Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; Bali ulimi wa mwenye haki ni afya.
Mdomo wa kweli utathibitishwa milele; Bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.
Hila imo mioyoni mwao wafikirio uovu; Bali wafanyao mashauri ya amani, kwao kuna furaha.
Mwenye haki hatapatikana na msiba wo wote; Bali wasio haki watajazwa mabaya.
Midomo ya uongo ni chukizo kwa Bwana; Bali watendao uaminifu ndio furaha yake.
Mwanadamu mwenye busara husitiri maarifa; Bali moyo wa wapumbavu hutangaza upumbavu.
Mkono wa mwenye bidii utatawala; Bali mvivu atalipishwa kodi.
Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; Bali neno jema huufurahisha.
Mwenye haki ni kiongozi cha mwenzake; Bali njia ya wasio haki huwakosesha.
Mtu mvivu hapiki mawindo yake; Bali mwenye bidii anazo mali za thamani.
Katika njia ya haki kuna uhai; Wala hakuna mauti katika mapito yake.