Yeremia Mlango 34 Jeremiah

Yeremia 34:1 Jeremiah 34:1

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, hapo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na jeshi lake lote, na falme zote za dunia zilizokuwa chini ya mamlaka yake, na kabila zote za watu, walipopigana na Yerusalemu, na miji yake yote, kusema,

Yeremia 34:2 Jeremiah 34:2

Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Enenda ukaseme na Sedekia, mfalme wa Yuda, ukamwambie, Bwana asema hivi, Tazama, nitatia mji huu katika mikono ya mfalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto;

Yeremia 34:3 Jeremiah 34:3

tena wewe hutaokoka mkononi mwake, lakini utakamatwa kweli kweli, na kutiwa katika mikono yake; na macho yako yatayatazama macho ya mfalme wa Babeli, naye atasema nawe mdomo kwa mdomo, nawe utakwenda Babeli.

Yeremia 34:4 Jeremiah 34:4

Hata hivyo lisikie neno la Bwana, Ee Sedekia, mfalme wa Yuda; Bwana asema hivi katika habari zako; hutakufa kwa upanga;

Yeremia 34:5 Jeremiah 34:5

utakufa katika amani; na kwa mafukizo ya baba zako, wafalme wa zamani waliokutangulia, ndivyo watakavyokufukizia; nao watakulilia, Aa, Bwana! Kwa maana mimi nimelinena neno hili, asema Bwana.

Yeremia 34:6 Jeremiah 34:6

Basi Yeremia, nabii, akamwambia Sedekia, mfalme wa Yuda, maneno hayo yote katika Yerusalemu,

Yeremia 34:7 Jeremiah 34:7

wakati ule jeshi la Babeli walipopigana na Yerusalemu na miji yote ya Yuda iliyosalia, na Lakishi, na Azeka; kwa maana miji hiyo tu ndiyo iliyosalia katika miji ya Yuda yenye maboma.

Yeremia 34:8 Jeremiah 34:8

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, baada ya wakati ule mfalme Sedekia alipofanya agano na watu wote waliokuwa katika Yerusalemu, kuwatangazia habari ya uhuru;

Yeremia 34:9 Jeremiah 34:9

ya kwamba kila mtu amweke huru mtumwa wake, na kila mtu amweke huru mjakazi wake, ikiwa yule mwanamume au yule mwanamke ni Mwebrania; mtu ye yote asiwatumikishe, yaani, asimtumikishe Myahudi, nduguye;

Yeremia 34:10 Jeremiah 34:10

na wakuu wote, na watu wote, wakati, waliofanya agano hilo, ya kwamba kila mtu amweke huru mtumwa wake na mjakazi wake, mtu ye yote asiwatumikishe tena; wakatii, wakawaacha.

Yeremia 34:11 Jeremiah 34:11

Lakini baadaye wakaghairi, wakawarudisha watumwa wale, na wajakazi wale, ambao wamewaacha huru, nao wakawatia utumwani wawe watumwa na wajakazi wao.

Yeremia 34:12 Jeremiah 34:12

Basi, neno la Bwana likamjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema,

Yeremia 34:13 Jeremiah 34:13

Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nalifanya agano na baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa, nikisema,

Yeremia 34:14 Jeremiah 34:14

Mwisho wa kila mwaka wa saba kila mtu na amweke huru ndugu yake aliye Mwebrania, aliyeuzwa kwako na kukutumikia miaka sita utamwacha atoke kwako huru, lakini baba zenu hawakunisikiliza, wala hawakutega masikio yao.

Yeremia 34:15 Jeremiah 34:15

Na ninyi mlikuwa mmegeuka, mkafanya yaliyo haki machoni pangu, kwa kumtangazia uhuru kila mtu ndugu yake; nanyi mlikuwa mmefanya agano mbele zangu, katika nyumba ile iitwayo kwa jina langu;

Yeremia 34:16 Jeremiah 34:16

lakini mlighairi, na kulitukana jina langu; kila mtu akamrudisha mtumwa wake na mjakazi wake, ambao mmewaweka huru kama walivyopenda wenyewe, mkawatia utumwani tena, wawe watumwa wenu na wajakazi wenu.

Yeremia 34:17 Jeremiah 34:17

Basi Bwana asema hivi, Hamkunisikiliza kumtangazia uhuru kila mtu ndugu yake, na kila mtu jirani yake; tazama, mimi nawatangazieni uhuru, asema Bwana, yaani, wa upanga, na njaa, na tauni; nami nitawatoa ninyi mtupwe huko na huko katika falme zote za dunia.

Yeremia 34:18 Jeremiah 34:18

Na watu hao waliolivunja agano langu, wasioyatimiza maneno ya agano lile, walilolifanya mbele zangu, wakati ule walipomkata ndama vipande viwili, wakapita katikati ya vipande vile;

Yeremia 34:19 Jeremiah 34:19

wakuu wa Yuda, na wakuu wa Yerusalemu, matowashi, na makuhani, na watu wote wa nchi, waliopita katikati ya vipande vile vya huyo ndama;

Yeremia 34:20 Jeremiah 34:20

mimi nitawatia katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na mizoga yao itakuwa ni chakula cha ndege za mbinguni, na cha wanyama wakali wa nchi.

Yeremia 34:21 Jeremiah 34:21

Na Sedekia, mfalme wa Yuda, na wakuu wake nitawatia katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na katika mikono ya jeshi la mfalme wa Babeli, waliokwenda zao na kuwaacheni.

Yeremia 34:22 Jeremiah 34:22

Tazama, nitawapa amri yangu, asema Bwana, na kuwarejeza kwenye mji huu; nao watapigana nao, na kuutwaa, na kuuteketeza kwa moto; nami nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, isikaliwe na mtu.